Monday, August 22, 2016

KUPATWA KWA JUA TAREHE 01 SEPTEMBA, 2016

                                                               Picha: Mfano wa kupatwa kwa jua

Hali ya kupatwa kwa jua ni tukio la aina yake linatokea pale ambapo miali ya jua hupungua hadi kutoonekana tena na kusababisha sehemu ya uso wa dunia kuwa giza wakati wa mchana. Muda wa kufunikwa kabisa ni dakika chache tu katika eneo husika.

Kupatwa kwa jua kunatokea wakati dunia, mwezi na jua vinapokaa kwenye mstari mmoja mnyoofu wakati mwezi unakuwa kati ya dunia na jua. Hali hiyo inapotokea kunajengeka kivuli cha mwezi kwenye uso wa dunia. Kivuli hicho hufunika sehemu  tu ya  uso wa dunia. Kutokana na hali hiyo kupatwa kwa jua kwa maeneo yaliyo mengi kunaonekana kwa watu wengi kama kupungua kwa mwanga wa jua.

2.Maelezo ya Kisayansi

Wanasayansi wanaelezea kupatwa kwa jua kama tukio linalotokea na kuonekana katika namna tofauti tofauti mfano; ni kupatwa kwa jua kikamilifu hali ambayo hutokea pale miali ya jua inapotea kabisa katika eneo husika kwa kipindi kifupi. Hali hii inapotokea eneo husika linakosa kabisa mwanga wa jua na kuwa giza.

Aina ya pili  ni kupatwa kwa jua kisehemu;  hii hutokea wakati eneo kubwa linapopata upungufu wa mwanga wa jua hali ambayo hupungua kadiri mtu anavyokuwa mbali na kitovu cha mstari wa kupatwa kwa jua. Kiwango cha upungufu wa mwanga wa jua hutegemea umbali mtu alipo kutoka kwenye kitovu cha kivuli kamili.

Aina nyingine ni kupatwa kwa jua kipete; hali hii inapotokea mwezi huzuia mwanga wa jua kufika kwenye dunia kwa vile huweka duara la kivuli cha mwezi kwenye dunia na hivyo mwanga wa  jua huonekana kama pete. Inatarajiwa kuwa aina hii ya kupatwa kwa jua ndiyo itakayojitokeza  tarehe 1 Septemba 2016 katika baadhi ya maeneo ya Bara la Afrika. Kwa hapa nchini hali hiyo inatarajiwa kujitokeza katika sehemu kubwa ya maeneo ya mikoa ya Nyanda za juu kusini magharibi na maeneo ya kusini mwa nchi.  Hata hivyo,  watu katika maeneo mengine ya nchi yaliyokaribu na ukanda huo wanatarajiwa kuona kupatwa kwa jua kisehemu yaani upungufu wa mwanga wa jua kwa dakika kadhaa, imetabiriwa takriban kakika tatu (3).  Jua linatarajiwa kupatwa wakati wa asubuhi kati ya saa tatu asubuhi na saa sita.

3. Athari zake kwa Hali ya Hewa.

Kwa ujumla hakuna athari zozote kubwa zinazotarajiwa kutokana na hali hiyo.  Hata hivyo, upo uwezekano wa kupungua kwa viwango vya joto katika maeneo ambapo kupatwa kwa jua Kipete kutajitokeza.  Kwa kuwa tukio hilo la kupatwa kwa jua huchukua muda wa dakika chache tu hali ya joto itapungua kwa haraka katika kipindi kifupi na baadae kuongezeka kurudi katika hali yake ya kawaida. Viwango vya kupungua kwa joto vitatofautiana kulingana na umbali kutoka eneo la kupatwa kwa jua

4. Upekee wa tukio la kupatwa kwa jua

Tukio hili hutokea au kujirudia mara chache sana katika eneo husika. Inakadiriwa kuwa inaweza kuchukua kati ya miaka 350 hadi 400 kwa hali hiyo kujitokeza tena katika eneo litakapotokea mwaka huu 2016. Hii ndio sababu kwa watu wa eneo husika na wanasayansi  hili ni tukio la muhimu na kumbukumbu muhimu ya maisha.

Mamlaka ya hali ya hewa inaendelea kufuatilia na itatoa taarifa za mabadiliko yoyote yanayoweza kujitokeza katika hali ya hewa kulingana na tukio hili la kupatwa kwa jua.



Dk. Agnes L. Kijazi
MKURUGENZI MKUU

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...